Diwani wa Kata ya Stesheni (Upande wa Kulia), Mhe. Ramadhan Mpilipili, tarehe 4 Februari 2026 ametembelea Shule ya Sekondari Stesheni kwa lengo la kuwapongeza walimu wa shule hiyo kwa kufaulisha vizuri wanafunzi katika Mtihani wa Taifa wa Kidato cha Nne.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mpilipili ametoa motisha kwa walimu kwa kuwapatia mifuko miwili ya ngano, sukari pamoja na majani ya chai, kama ishara ya kuthamini jitihada na mchango wao katika kuinua taaluma.

Akizungumza na walimu, Mheshimiwa Diwani amesema anawapongeza kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa ushirikiano, hali iliyoiwezesha Shule ya Sekondari Stesheni kushika nafasi ya pili kiwilaya, ikizidiwa kwa pointi mbili pekee na Shule ya Sekondari Nachingwea Girls, ameeleza kuwa mafanikio hayo ni ya kupongezwa zaidi ikizingatiwa kuwa Nachingwea Girls ni shule ya bweni, huku Stesheni ikiwa shule ya kutwa.

Kwa upande wake, Afisa Elimu Kata amepongeza hatua ya Diwani kutoa motisha kwa walimu, akisema ni faraja na chachu ya kuongeza bidii kazini, ameeleza kuwa shule hiyo imepata matokeo mazuri kwa kufaulisha kwa GPA ya 2.5 bila mwanafunzi hata mmoja kupata daraja la sifuri, huku Shule ya Sekondari Nachingwea Girls ikipata GPA ya 2.7.
Amesisitiza kuwa matokeo hayo ni ushahidi wa mshikamano na juhudi za pamoja kati ya walimu, wanafunzi na wadau wa elimu katika kata ya Stesheni.
Copyright ©2018 Nachingwea District Council. All rights reserved.