Mei 5, 2025 Kamati ya Mipango na Fedha ya Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea imefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Kata za Chiumbati shuleni na Naipingo, ikilenga kuhakikisha miradi inakamika kwa wakati.
Katika ziara hiyo, kamati imetembelea mradi wa ujenzi wa shule ya sekondari katika Kata ya Chiumbati wenye thamano ya shilingi milioni 560, pamoja na bweni la wavulana katika Shule ya Sekondari Rugwa Boys lenye thamani ya shilingi milioni 147, kamati katika bweni hilo imelenga kujiridhisha na hatua ya umaliziaji kabla ya mzabuni kulipwa fedha zilizobaki kufuatia maagizo yaliyotolewa katika ziara ya awali.
Kamati ilikagua ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Naipingo yenye thamani ya shilingi milioni 50 za mapato ya ndani, pamoja na jengo la kisasa la utawala lenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 3.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mheshimiwa Adinan Mpyagila, amewapongeza watendaji wa Halmashauri wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya, Mhandisi Chionda Kawawa kwa usimamizi mzuri na utekelezaji madhubuti wa miradi, pia amehimiza kuendelea kushughulikia changamoto ndogondogo zilizosalia ili kuongeza tija na kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati uliopangwa.
Mheshimiwa Mpyagila amewashukuru madiwani kwa kusimamia miradi hiyo katika maeneo yao, na kuwapongeza wananchi kwa ushirikiano wao katika kufanikisha maendeleo ya Wilaya ya Nachingwea.
Kwa pamoja, wajumbe wa kamati hiyo wameonesha kuridhishwa na hatua za utekelezaji wa miradi hiyo, na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano katika kufanikisha malengo ya maendeleo kwa wananchi.
Copyright ©2018 Nachingwea District Council. All rights reserved.