Leo, Mei 2, 2025, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Zainab Telack, amewapongeza walimu wa Mkoa wa Lindi kwa kazi kubwa, moyo wa kujituma na weledi waliouonesha katika kuhakikisha ufaulu wa wanafunzi unaongezeka, hususan katika mitihani ya kitaifa na upimaji wa mara kwa mara. Hafla hiyo ya utoaji wa Tuzo za Elimu ilifanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Likangara, ya Wilaya Ruangwa.
Mhe. Telack amesema mafanikio hayo yametokana na mshikamano, nidhamu na moyo wa kujitoa wa walimu. Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha vipindi vya dini vinafanyika shuleni ili kujenga maadili mema kwa wanafunzi.
“Niwapongeze sana walimu wetu. Mmefanya kazi kubwa kwa moyo. Mmeonesha ufaulu si bahati bali ni juhudi. Changamoto ndogondogo msiogope, ziletwe kwetu ili tuweze kuzitatua na kuhakikisha mnapata njia nzuri ya kupita,” amesisitiza Mhe. Telack.
Katika hafla hiyo, walimu, wanafunzi, shule na viongozi mbalimbali wa elimu walitunukiwa tuzo na zawadi kwa kutambua mchango wao katika kuinua kiwango cha elimu. Mhe. Telack amehimiza kuwa tuzo hizo ziwe chachu ya kuongeza bidii ili mwakani ufaulu uzidi kuimarika, na zoezi hilo liwe endelevu katika kila mwaka.
Copyright ©2018 Nachingwea District Council. All rights reserved.