Tarehe 6 Juni 2025, Mohamed Kaidi Afisa Kilimo kutoka Bodi ya Korosho Makao Makuu Mtwara , ameshiriki mahojiano maalum katika kipindi cha Amka na 90.9 kupitia Kituo cha Redio Nachingwea FM.
Katika mahojiano hayo, ameeleza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Bodi ya Korosho kuhakikisha wakulima wanapata pembejeo kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa. Ametaja kuwa tayari wameajiri maafisa ugani 500 nchini kote, huku lengo likiwa kufikia 1,000. Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea imeongoza kwa Mkoa wa Lindi kwa kupata maafisa ugani 41.
Ametoa wito kwa wakulima wote kusajili mikorosho yao, ikijumuisha hata ile michanga, kwa lengo la kuongeza ufanisi wa usimamizi wa zao hilo. Aidha, ameonya kuhusu udanganyifu unaofanywa na baadhi ya wakulima au viongozi, akisisitiza kuwa ukaguzi unaendelea na hatua kali zitachukuliwa kwa watakaobainika. Amesisitiza umuhimu wa wakulima kutoa taarifa sahihi kwa wakati.
Kuhusu matumizi ya viuatilifu, Afisa huyo amekemea vikali tabia ya kuchanganya dawa bila maelekezo ya kitaalamu, akieleza kuwa ni hatari kwa afya, mazingira na mazao.
Kwa msimu huu wa kilimo, Bodi ya Korosho imepanga kusambaza tani 40,000 za salfa (sulphur) pamoja na lita milioni 3.8 za dawa na viuatilifu kote nchini. Hadi sasa, Wilaya ya Nachingwea imeshapokea zaidi ya Mifuko elfu 59 za salfa na lita 75,000 za viuatilifu , salfa zaidi ya asilimia 60 ya mgao wake.
Ametambua kuwa changamoto ya upatikanaji wa viuatilifu ilisababishwa na ongezeko la mahitaji kutoka kwa mazao mbalimbali, lakini kwa sasa vimeshawasili na vinaendelea kukaguliwa kabla ya kuwafikia wakulima. Ameeleza kwa kuridhika kuwa mwaka huu pembejeo zimewafikia wakulima kwa wakati.
Aidha, amefafanua kuwa asilimia 90 ya pembejeo za maji tayari zimeshawasili katika ghala kuu la Mtwara, na kuanzia wiki ijayo, usambazaji rasmi kwa AMCOS zote utaanza, kuhakikisha kila mkulima aliyebaki anazipata kwa wakati.
Copyright ©2018 Nachingwea District Council. All rights reserved.